Blog yenu ya wananchi yenye habari motomoto za kijamii, Blog yenye kuelimisha, kuburudisha na kufurahisha. Wapenzi na wasomaji wetu tunaomba ushirikiano wenu ili kuendeleza Blog yetu, kwa pamoja tunaweza kuleta mabadiliko ya kweli.

Thursday, February 23, 2012

Maisha Na Malengo Yako-Tz Yangu

Mwanzo wa mwaka huja na mwamko mpya, mategemeo mapya, matumaini mapya,  mipango na malengo mapya. Wengi wetu huanza kwa nguvu nyingi sana mwanzo wa mwaka, kwa sababu , mwanzo una mwamko wake. Lakini wote yatupasa kufahamu ukwelu kwamba;  katika maisha,  haijalishi umeanzaje au umetoka wapi bali umemalizaje.
Maisha ni kama marathoni, haswa katika huu  mwanzo wa mwaka huwa ni nafasi pekee  kwa wengi wetu kutathimini juu ya malengo yetu na hata kutafuta kujua malengo yetu mapya; na cha zaidi  ni kuanza na stamina au nguvu mpya kwa ajili ya mwaka mzima.
Mwanzo wa mwaka huwa ni muda  muafaka ambao hutufanya sisi kujichunguza wenyewe au kujiuliza yale tuliyoyafanya mwaka uliopita yametufikisha wapi na yako wapi. Mwaka mpya hauji na  kalenda mpya pekee,  bali  ni mtu mpya, malengo mapya au yaliyonolewa zaidi na  mipango mipya.
Maisha ni safari ndefu na zaidi ni shule, na Dunia ina mengi  sana – na pia sitaweza kupuuza ukweli ya kwamba tunaishi katika dunia yenye wanadamu waliochanganyikiwa kwa kiasi Fulani kwasababu dunia yenyewe imechanganyikiwa. Tunaishi katika Dunia ambayo , mtu usipokuwa na malengo yako binafsi utabebwa na matukio ya maisha.
Na ili kuanza upya ni vema kuwa na ufahamu mpya na njia mpya za kuyafikia malengo ulionayo kwa mwaka mpya. Binadamu tunayo mengi tusiyoyajua kuhusu sisi, na tunachokijua ni kidogo sana kuhusu sisi na kwa bahati mbaya mara nyingi wengi wetu hufeli kufahamu zaidi juu ya uwezo tulionaona ndani yetu hata kufa bila kujua tulichonacho, rafiki yangu , fahamu ya kuwa tunayo makubwa sana ndani yetu, na wengi wetu hatujui au hatutaki kuamini kuwa ukuu huu umo ndani yetu.
Matukio mbalimbali ya dunia yametufundisha na kutufanya tuamini mengi sana ambayo sio sahihi kuhusu sisi na kutufanya kusahau ukweli wa ukubwa uliopo ndani yetu. Mimi naamini kabisa kuwa tukiamua na kumaanisha  kujitafuta, kujijua, kujifunza, kujiendeleza ili tuweze kuwa sisi, tutapata uhalisi wetu ambao tumeupoteza kwa kutokujua. Sisi ni zaidi ya jinsi tulivyo, ni zaidi ya jinsi ya tunavyojifahamu na tunavyoishi.
Maisha ni magumu sawa lakini ulichonacho ni zaidi ya mazingira, unayo nguvu ya kuyaendesha na kuyasababisha mazingira yako. Haijalishi unaishi vipi, una elimu ipi na umekulia wapi dunia ni yako, maisha ni yako na ni uamuzi wako – amua leo  kuishi kiukweli kuhusu wewe na kusababisha ya kwako.  Kwa mwanzo wa mwaka huu tafadhali fanya yafuatayo:
1.     Jifunze kutoka jana: Ingawa mambo ya jana yamepita lakini ni muhimu wewe kujifunza makosa yote uliyoyafanya jana,mfumo upi uliokufelisha jana na nini ufanye kuyarekebisha hayo sasa. Usilie kwa yaliyopita jana, bali weka mkazo kwa yale yatakayokuja sasa. Yaliyopita yamepita na huwezi kuyabadili ila ni faida kwako kwani waweza kujifunza kupitia hayo. Jana bado ipo kwa maisha yako ili upate faida ya kujifunza.Sema asante jana.

2.     Jifunze kufurahia na  kuishi leo: Maisha yako halisi yanaendelea leo, hivyo basi ishi leo, furahi leo, cheka leo, tafuta leo, jikubali leo. Hata kama unadhani mazingira yako ya leo hayajakaa poa, jifunze kuishi leo kwa ulichonacho leo huku macho yako yakiangalia na kujipanga kwa ajili ya  kesho.
3 Jifunze kuangalia na kujipanga kwa ajili ya kesho:  Katika maisha haijalishi upo katika hali gani au mazingira gani  bali kule unakokwenda. Hata kama una hali ya aina gani, jifunze kuangalia mbele,  kuwa na matumaini ya kesho. Kesho yako itaonekana tu ukiamua kuitengeneza katika akili na imani yako , na hata zaidi , kimatendo. Kumbuka kuwa macho yaliwekwa mbele ili kuangalia na kwenda mbele, jifunze kuangalia mbele, jifunze kuangalia kesho kwa matumaini na shauku kubwa zaidi kuanzia  leo.
4.     Amua kubadilika wewe kwanza: Badilika ili kufanya vizuri zaidi kile unachokifanya au kingine unachotaka kukijua, badilika ili utoe matokeo mazuri mwisho wa mwaka, amua kujiendeleza kwa kusoma vitabu vinavyoweza kukuendeleza na si kukupumbaza akili. Na ukumbuke kuwa ukitaka mabadiliko yoyote maishani badilika wewe kwanza.
5.     Fanya malengo yako kuwa sehemu ya maisha yako ya kila siku: Kumbuka kuwa dunia hii imechanganyikiwa. Ni rahisi sana kubebwa kama takataka na pepo na ukaishia kuishi maisha ya wengine. Ni rahisi kupoteza ukweli wetu kuhusu sisi. Yapo mambo mengi yanayotufanya tupoteze muda wetu duniani na zaidi yanayoweza kutufanya tusiongee na mioyo yetu. Usipong’ang’ania kuishi malengo yako , usipousikiliza moyo wako dunia itakupoteza, kwani  haina huruma kama usipoamua kujisimamia. Watu wengi wenye mafanikio kila siku, usiku na mchana wanahangaika kuyafikia malengo yao zaidi. Wanautumia muda wao wote kuyafikia malengo yao na hawachoki. Jifunze kila siku kufanya yale yatakayokufikisha katika malengo yako.
6.     Usikate tamaa: Maisha yanachanganya, na mara nyingi huonekana kuwa magumu lakini inawezekana kabisa kufanikiwa; haswa ukijidhatiti kuyafikia unayoyataka. Fahamu kuwa, kuishi kwako duniani ni kwa muda tu,na ndoto yako na malengo yako ni kama sababu ya kuwepo kwako. NI UHAI WAKO. Hakuna kitu chochote kizuri duniani kinachopatikana bila kujitoa. Ukitaka cha kwako kifanikiwe na kutambulika, amua kujitoa mpAka kukipata na usikate tamaa njiani mpaka kipatikane. Tafadhali usikate tamaa, usikate tamaa.

Nahitimisha kwa kusema kuwa, Dunia hii inayo nafasi kwa yeyote anayetaka kufanikiwa na yupo tayari kutoka moyoni, akilini mwake, kimatendo na hata kimwili kuyafikia malengo yake; wapo watu wengi waliofanikiwa na wanaofanikiwa kila mwaka – na hii si kwamba wao ni watu pekee ambao walioletwa duniani ili kula mema ya dunia peke yao, bali tofauti yao ni kwamba wameamua kuyashikilia malengo yao bila kukata tamaa , huku kila siku wakitaraji kufanikiwa. Amua kuishi kiushindi leo – badilika kwanza wewe kabla haujaona mazingira yako yanaanza kubadilika.
Geophrey  Tenganamba
Mungu Ibariki Tanzania
Kwa mawasiliano zaidi na ushauri katika maisha biashara, semina na vitabu vya Geophrey Tenganamba  piga simu:+255714477218

No comments:

Post a Comment

Msomaji wetu hakikisha unaheshimu mila na tamaduni za mwafrika,lugha zenye utata au kumkashifu mtu haitapendeza kuonekana kwenye post.Kumbuka vigezo na masharti ya comments kuzingatiwa.Asanteni sana kwa kuwa nasi kwenye blog yenu.