Blog yenu ya wananchi yenye habari motomoto za kijamii, Blog yenye kuelimisha, kuburudisha na kufurahisha. Wapenzi na wasomaji wetu tunaomba ushirikiano wenu ili kuendeleza Blog yetu, kwa pamoja tunaweza kuleta mabadiliko ya kweli.

Wednesday, February 29, 2012

Taifa la waliao, wakilia na kuliwa, nani atawafungua?

M. M. Mwanakijiji

LIPO taifa sitalitaja ambapo watu wake huliwa huku wanalia na wale wanaowala nao wanaliwa huku wakilia na kuliliana huku na wao wenyewe wakililiwa. Taifa hili - ambalo sitalitaja linaongozwa na watu wanaopenda kula sana.
Wanakula kila kilichopo mbele yao na wanakula kama wasiojua kushiba. Wanakula hata uji wa mgonjwa, wanakula hadi vya watoto!
Wanakula huku hakuna wa kuwauliza kwani hata wale ambao wanapaswa kuwauliza na wenyewe wanapiga mahesabu ya jinsi gani wataingia mezani nao kula! Ni taifa la walao na wale waliwao!
Mtu yeyote anapotembelea taifa hili nisilolitaja anaweza kuona mara moja tofauti kati ya wale wanaokula, wanaoliwa, wanaotaka kula na wale wanaolilia kutaka kula au wanalia wakiliwa au vya kwao vikichukuliwa kuliwa.
Wapo amba kwenye hili taifa lisilo na jina, wameshikilia masufuria na mabakuli makubwa ya kula wakilia kwa sauti za kukoroma (zenye mikwaruzo ya kuudhi) “ongeza ongeza!” wakiwalilia watu wasio na uwezo wa kuwapa cha nyongeza. Wafanyakazi na wakulima katika taifa hili wanaambiwa tena kwa kupigiwa kelele “fanyeni kazi kwa bidii na maarifa” ili pato liongezeke.
Wasichoambiwa maskini hawa wa Mungu ni kuwa wanaambiwa waongeze uzalishaji ili mabakuli ya walaji yazidi kuongezewa. Songombingo huja pale maskini hawa wenye kuliwa wanapoamua siku moja na wao waamue kudai nyongeza kidogo ya kula hata kama ni tumifupamifupa.
Walaji wakubwa huja juu; wanang’aka na wakati mwingine na vitisho! Nilisimuliwa kisa kilichotokea kwenye hiyo nchi nisiyoitaja pale kundi moja la walaji wadogo wadogo lilipojaribu siku moja kutishia kuacha kuwapikia walaji wakubwa!
Msimamizi mkuu wa walaji wakubwa alichukizwa sana na aliamua kuwapiga mkwara hadharani wale walaji wadogo na kuwaambia wasikubali kutumiwa na watu wabaya hata wakafika mahali wakakataa kuwapikia walaji wakubwa.
Katika mkutano wake na Wazee wa Walaji Mlaji yule mkubwa alizungumza kwa hasira sana na kuwaambia kuwa wakiendelea kutishia maslahi ya walaji watapigwa virungu. Maskini wa Mungu wale wapishi wakuu walibakia wanatetemeka hasa walipokumbushwa kisa cha ndege fulani, kisa ambacho kwa kweli kiliwalazimisha kufikiria mara mbili.
Walaji wakubwa waliendelea kula na kutafuna huku wakicheua mafuta, wakikumbatiana na kupongezana huku wakifanya mpango mwingine wa kujiongezea kula zaidi. Kilichowatibua wanaoliwa zaidi ni siku ile ambapo walaji wakubwa walipoamua kujiongezea ulaji zaidi huku wakiwaambia wananchi wa taifa lile nisilolitaja kuwa taifa lao liko kwenye hali mbaya ya uchumi. Wakaamua kujiongezea ulaji huku wakitetea kuwa walaji wote wakuu wamekubaliana kula!
Ndipo kundi jingine la watengeneza chakula cha walaji wakubwa lilipoamua na lenyewe kuomba kidogo liongezewe kwenye sinia lao la ulaji. Ndugu zangu hawa walikataliwa kwa mbinde na upinde, kejeli na dharau. Lilikuwa kosa ambalo walaji wakuu hawalikutarajia. Kwani wanaohudumia walaji wakubwa wakaamuka kugoma!
Kama utani hivi. Walaji wakuu walikuwa na uhakika wa kutosha tu kuwa walaji hawa wadogo hawana umoja na hawawezi kusimamia mgomo kwa muda mrefu. Oh, walijikuta wanashangazwa pale ambapo walaji wale walipong’ang’ana wakang’ang’ania!
Ndipo mmoja wa walaji wakubwa alipojitokeza kwenye runinga akiwa amekasirika na akiwa amezungukwa na walaji wengine mahiri wote wakiwa na nia moja kuwalazimisha wapishi warudi jikoni! “Msiporudi kutupikia mtajifukuzisha kazi” alitamka mlaji mkuu msaidizi. Kesho yake hakuna aliyerudia! Mambo yalianza kuwa mabaya kwenye taifa la lile nisilolitaja.
Waliokuwa wanaliwa sana na ambao walijikuta wanazidi kulia wakati mgomo ukiendelea walipoamua kufanya kweli. Wakajitokeza na kuandaa umati kuwapinga walaji wakubwa! Wakubwa wakashtuka kwani hilo hawakulitarajia. Walitarajia kuwa wakipiga mkwara, mabomu na vitisho basi wanaoliwa watanyamaza kwani kwenye taifa lile mikwara hufanya kazi sana.
Huku nyuma mlaji mkubwa akisema kitu basi watu hufyata mkia. Haikuwa hivyo safari hii. Wanaoliwa hawakuwa tayari kukaa kimya; waliamua kubanana na watawala wao kwenye taifa hili nisilolitaja.
Mambo yalipozidi kuwa magumu na wanaoliwa zaidi walipozidi kulia na kuanza kupiga mayowe ndipo walaji wakubwa walijikuta hawana jinsi bali kukaa na wapishi wao kujaribu kutafuta suluhu. Wakakubali kuwaongezea kidogo kwenye masinia yao. Lakini hawakuwa tayari kuwanyanganya ulaji walaji wenzao wakubwa!
Na uwezekano wa walaji wale wakubwa waliosababisha tafruku hiyo kuhamia na kupelekwa kwingine kula ni mkubwa kwani kwenye taifa la walaji hakuna anayenyang’anywa sahani! Wanahemishwa meza au viti! Ukihamishwa meza unaweza kupelekwa kwenye kula kwa kunyemelea lakini ukihamishwa kitu umehamishwa mkao wa kula tu! Kula kunaendelea!
Ni mpaka pale wale waliwao watakapoamua kukataa kuwa sababu ya kula kwa wale walao ndipo mabadiliko ya kweli yanaweza kuanza kutokea. Vijana wanaojitahidi kila siku kufanya kazi watakapokataa kuwa sehemu ya mfumo wa kuliwa ambao wenye kula hula wakirithisha hadi watoto wao kula watakapokataa kuwa watetezi wa mfumo huo wa ulaji ndipo vijana wa taifa hilo ambalo sijalitaja watakapoanza kutafuta sehemu yao katika maisha ya nchi yao.
Walaji watakapokataliwa kula au kujiongezea vya kula ndipo wale wanaoliwa nao watapata nafasi ya kutafuta chakula! Nje ya hapo, walaji wakubwa, watetezi wa walaji na chama chao kikuu chao ulaji wataendelea kula bila kuulizwa huku mamilioni ya wananchi wenzao wakiendelea kubakia kunawa mikono na kuitwa kuja kutoa vyombo!
Wale wengine ambao wamegundua kuwa nje ya chama cha walaji hakuna nafasi wanajikuta wanaamua kuanza kuimba wimbo wa kusifia walaji ili na wao hata kama hawatakula sana wawekwe mahali ambapo wanaweza kuambulia makombo! Kumbuka, makombo ya walaji wakubwa ni chakula tosha kwa maskini mwombaji aliyeko kwenye taifa lile nisilolitaja!

Tanzania daima

No comments:

Post a Comment

Msomaji wetu hakikisha unaheshimu mila na tamaduni za mwafrika,lugha zenye utata au kumkashifu mtu haitapendeza kuonekana kwenye post.Kumbuka vigezo na masharti ya comments kuzingatiwa.Asanteni sana kwa kuwa nasi kwenye blog yenu.