Blog yenu ya wananchi yenye habari motomoto za kijamii, Blog yenye kuelimisha, kuburudisha na kufurahisha. Wapenzi na wasomaji wetu tunaomba ushirikiano wenu ili kuendeleza Blog yetu, kwa pamoja tunaweza kuleta mabadiliko ya kweli.

Friday, April 6, 2012

Poleni watu wa Mtera kwa kuanguka mikononi mwa chizi

 
Mbunge wa Mtera CCM, Livingstone Lusinde aka Kichaa akirapu rapu zake za matusi  ya nguoni kule Arumeru Mashariki hivi karibuni.

KAMPENI zilizopita za uchaguzi mdogo wa Arumeru Mashariki, zilifichua mambo mengi hasa uhovyo wa siasa na viongozi wetu. Mambo yalianza na wazee wazima Benjamin Mkapa, rais mstaafu, kujivua nguo kwa kujifanya msemaji wa ukoo wa marehemu Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere ambaye alimtengeneza na kumnadi Mkapa lakini baadaye akamwangusha vibaya kiasi cha kufa akiwa analilia Watanzania wake.

Nani mara hii kasahau maneno ya mke wa marehemu, Mama Maria Nyerere aliyesema kuwa maneno ya mwisho ya mumewe yalikuwa, "Nawalilia Watanzania wangu"?

Hii maana yake Mwalimu alikufa na roho iliyojikunja; ikizingatiwa Watanzania aliokuwa akiwalilia walikuwa kwenye mikono ya mtu wake lakini aliyeonyesha wazi kuwa wa hovyo kisera.

Mwingine aliyejivua nguo ni mzee Stephen Wassira, Waziri wa Uhusiano na Uratibu Ofisi ya Rais ambaye alianzisha ligi ya matusi na uongo kwenye kampeni kiasi cha kugeuka kuwa uwanja wa wahuni wa chama chake kuja kuonyesha uhuni na uhovyo wao. Wassiara alikaririwa akimtuhumu katibu mkuu wa CHADEMA, Dk. Willibrod Slaa kula pesa ya maandalizi ya ujio wa Papa John Paul II mwaka 1990, madai ambayo yalipingwa vikali na Kanisa Katoliki ambalo bosi wake ndiye alikuwa akitembelea Tanzania.

Rais wa TEC, Askofu Mkuu Juda Thaddeus Ruwa'ichi alimjibu Wassira kwa maneno haya, “Ukiona mwanasiasa anakurupuka na kuanza kumchafua mwenzake ujue amefilisika, vitendo hivyo vinaonyesha udhaifu kwa nchi katika nyanja za siasa,”

Hayo ya Mkapa na Wassira yalikuwa cha mtoto au tuseme ufunguzi tu. Maana baba yao katika ligi hii ya matusi, Mbunge Livingstone Lusinde wa Mtera (CCM) alikuwa hajaja kumaliza kazi hii aliyotumwa na chama chake. Alikaririwa akitamka maneno ambayo si vizuri kuyarudia na wala hayafanani na mtu wa umri na wadhifa wake kama mbunge mwakilishi wa wananchi. Hivi mtu anayeweza kusimama kwenye jukwaa la siasa kutangaza sera akatangaza matusi tena kwa kuiga maneno ya vikundi vya maigizo, umuweke kundi gani? Zamani wengi tulikuwa tukikwazwa na salamu za Mkapa za kihuni za “MAMBO” bila kujua kuwa kumbe kuna wahuni zaidi.

Lusinde alikaririwa akisema kuwa kama CHADEMA ni vichaa wa kurogwa basi yeye ni wa kuzaliwa. Ni bahati mbaya na hasara kuwa na viongozi aina ya Lusinde. Je, ilikuwaje watu wa Mtera wakamchagua chizi anayekiri kuwa chizi tena tangu kuzaliwa? Je, alipitaje kwenye mchujo au ni yale yale ya wananchi kuchoka utawala wa mtu mmoja na wa kurithishana kutokana na ukweli kuwa mbunge wao wa zamani John Malecela alikuwa amewachosha kwa kukaa madarakani kwa muda mrefu?

Nashindwa kujua mantiki ya kumchagua mtu wa hovyo na kichaa kama huyu anayeweza kusimama jukwaani na kuwadhalilisha wenzake tena mbele ya watoto wadogo akionyesha uhodari wa kuchambua mavazi ya wenzake badala ya matatizo ya anaowawakilisha?
Hivi mbunge anaposimama jukwaani na kugeuza mdomo wake sehemu ya kutolea uchafu, tena mbele ya kadamnasi na watoto, anajenga picha gani? Je, huu si ushahidi tosha kuwa CCM imeishiwa kiasi cha kushabikia uhuni na mipasho ya kipumbavu? Je hii si kuigeuza CCM kuwa Chama Cha Matusi? Hata waimbaji wa taarabu za matusi na hata rap wana afadhali kwa vile wayafanyayo ni saizi yao.

Sijui kama Lusinde anasoma hata magazeti zaidi ya yale ya udaku kama alivyothibitisha kwa kauli zake za kichovu na kiwendawazimu. Je, maneno na tabia vya Lusinde vinakisaidiaje chama chake zaidi ya kukibomoa? Maana ukiangalia kuzodolewa, kwa mfano, kwa Wassira hata Mkapa ni ushahidi tosha kuwa CCM iko pabaya na imeishiwa.

Je yote haya ni matokeo ya kuua maadili na kuingiza madili kwenye nafasi yake? Maana kwa nchi yenye kufuata sheria na kanuni za maadili, tume ya uchaguzi (NEC) ilipaswa kutoa tamko hata karipio mara moja Lusinde alipogeuza kampeni uwanja wa kushindanisha ukichaa na matusi ya nguoni.

Hivi mtu anayeweza kuwaita wanaume wenzake mashoga na wajawazito ana akili kweli? Heri angeishia pale. Wenye mtindio wa akili wenzake wangedhani amewajibu wapinzani japo siyo. Nani mara hii alivyowaambia wapiga kura kuwa yeyote ambaye hataichagua CCM ni mjamzito? Je, ujauzito ni ugonjwa? Hivi bila ujauzito mama yake angemzaa kweli? Je kutukana watu kwa kutumia ujauzito si kuwadhalilisha wanawake na mama yake akiwamo? Maana huo ujauzito usio na baba maana yake ni umalaya.

Maneno ya Lusinde ni ushahidi kuwa hakupata malezi mema wala elimu ya kutosha kiasi cha kujenga taswira kuwa huenda alizaliwa mitaani. Maana hata tofauti na wahuni wanaopiga debe kwenye mabasi ya daladala wala wauza mitumba Mtaa wa Kongo. Heri ya wao wamefukarishwa na akina Lusinde kuliko Lusinde anayelipwa kodi ya wananchi kwa kuchafua maadili akilinda na kutetea uozo na mgando wa mawazo. Tena uoza wenyewe utawala wa kurithishana kama walivyoonyesha kwenye kuteua wabunge wa Jumuia ya Afrika Mashariki!

Kama siyo CHADEMA kuchelea kukimbizana na kichaa, ilifaa afunguliwe mashitaka. Hata hivyo, kwa kauli za watajwa watatu, kama CHADEMA watashindwa basi wana kila sababu ya kwenda mahakamani na kudai uchaguzi haukuwa huru na wa haki. Maana haki na uhuru ni heshima na si kashfa tena za kuzua na matusi. Laiti Lusinde angewatuhumu CHADEMA mambo ya kweli, hakuna ambaye angehangaika naye. Litakuwa jambo la ajabu na hatari kama CCM na Tume ya Uchaguzi hawatamchukulia hatua za kinidhamu tena za wazi Lusinde.

Kuna haja ya wachambuzi wa mambo kudodosa na kupata historia ya Lusinde ili apewe msaada na wale waliofanya kosa kumwamini wadhifa wa heshima kama ubunge. Kimsingi lugha na matusi ya Lusinde yamewadhalilisha wabunge wote hasa wa chama chake na uongozi mzima. Hivi kama Lusinde ana mke na watoto hata wazazi wake sijui amewaumiza kiasi gani kwa kujivua nguo hadharani hivyo? Poleni sana watu wa Mtera. Huenda ni yale yale kuwa atukanaye wakubwa haishii na mmoja.

Alimtukana John Malecela akazoea sasa anataka kumtukana kila apitaye. Si ajabu akitofautiana hata na mwenyekiti wake hatakosa kumfurumshia mitusi ya nguoni kama alivyozoeshwa na chama chake. Poleni wapiga kura wa Mtera kwa kudhalilishwa na Lusinde ambaye aliwakilisha matusi badala ya heshima na matatizo yenu.
Chanzo: Tanzania Daima Aprili 4, 2012.

Mbunge ‘Chichim’ alivyomwaga mitusi Arumeru

LEO tumeamua kukaa kikao cha wanakijiwe wote ili kumjibu chizi mmoja aitwaye mheshimiwa japo sisi si machizi. Kama mkituona machizi shauri yenu. Tunaweza kuonekana walevi kutokana na kunywa kahawa na shida nyingi lakini bado si machizi kama Leavingstorm Lushinde chizi nambari wani wa Chama Cha Machizi (CCM).

Mie kama mwenyekiti naanzisha mjadala.
Nilikohoa kidogo na kuanza, “Waheshimiwa wanywa kahawa, kwanza naona mmechukia kutokana na matusi yalivurumishwa na mbunge wa ndugu yetu na rafiki yetu Mbwamwitu ambaye ni mpiga kura wa jimbo la Mtela,”

Wote kwa pamoja wanatikisa vichwa wakiashiria kukubaliana na pwenti yangu. Naendelea, “Mie leo si msemaji bali mwezeshaji. Hivyo naomba rasmi nifungue kikao hiki kitukufu ambacho licha ya kumjadilli huyu bwana kitatoa maazimio.”

Mbwamwitu anaamsha mkono na ninamruhusu arambe mic. Anaanza, “Ndugu zangu nashukuru sana kwa kuliona hili na pole zenu nimezipokea ingawa bado roho inaniuma. Hata hivyo msishangae sana. huyu jamaa kama alivyosema kweli ni chizi na aliwahi kukamatwa mara nyingi kwa makosa ya kuvuta bangi, udokozi na mazambe mengine mengi. Hivyo nina wasi wasi alipokuwa akiwekwa ndani mara nyingi, huenda lolote limemtokea na ndiyo maana anawasingizia wenzake kufanyiwa mchezo mbaya kama alivyowahi kufanyiwa.”

Kabla ya kuendelea Mchunguliaji anakula mic, “Hakuna kitu kimenikera kama jamaa kuwaita wenzake mashoga kiasi cha kutufanya tuamini yeye ndiye. Halafu anawatukana watu eti wana mimba, kwani mama yake alimzaa bila kubeba hiyo mimba? Huyu jamaa inaonekana anawadhalilisha akina mama akiwamo mama yake wallahi,”

Wakati Mchunguliaji akimwaga usongo wake, Mzee Kidevu anadandia, “Huyu jamaa kweli chizi nimeamini. Kwanza, huyu chizi kihiyo hajui hata Kiswahili. Mnakumbuka aliposema eti dokta Silaha aliposema ana uchungu na nchi hii eti alimshagaa mwanaume anawezaje kuwa na uchungu? Kwani uchungu ni wa kuzaa tu?”

Mara Mipawa anachomekea, “Jamaa ana ugomvi na mimba huyu. Huenda kichaa chake kinachukia mimba.”

Watu hawana mbavu wanacheka ingawa habari yenyewe si ya kuchekesha zaidi ya kuhuzunisha. Mara Mbwamwitu anakatua mic tena, “Basi mwenzenu nina uchungu naye. Laiti nikikutana naye kwenye kiza ataipata hiyo mimba anayowapa wenzake. Huyu inaonakana anataka kupewa mimba.”

Msomi Mkatatamaa aliyekuwa kimya muda wote aliamua kutia guu, “Jamani msijipasue vichwa. Kimsingi, Lushinde alichofanya ni kuthibitisha madai ya siku nyingi kuwa chama chake kimeishiwa sera. Kilianza na usanii, kikachemsha. Kilidandia uongo, kimechemsha. sasa kimeona haitoshi kimedandia matusi.” anavuta kombe lake na kubwia kahawa na kuendelea, “Matusi ya Lushinde kimsingi si ya kuwahuzunisha wala kuwalenga wapinzani bali chama chake na viongozi wake waliokuwa wakichekelea alipokuwa akitumia mdomo wake kutoa haja kubwa. This annoyed me to death so to speak.”

Anakatua kashata na kuendelea. “Kila mtu kwake shoga. Inakuwa vigumu kujua huyu bwana kwanini anapenda sana ushoga na kuchukia mimba,” Msomi Mkatatamaa alizidi kuchanja mbuga kwa taaluma na busara zake baada ya wazee kumwambia apunguze hasira kuongea kikameruni hata kama alikuwa akiongelea habari za mkameruni mhishimiwa.

Aliendelea, “Hakika wazazi wake, mke wake, watoto wa Mkameruni Lushinde wamekula hasara. Anavyowatia aibu sina hamu. Hata yule mheshimiwa Sonko wa Nonihino huvuta bangi, kunywa gongo na kupayuka lakini hajawahi kuona mdomo choo kama wa Lushinde. Maana kama sera basi chama chake cha Matusi (CCM) kimepata mpiga debe. Ila itakuwa muujiza kama walengwa wa makombora ya Lushinde wasipomfikisha mhakamani. Sisi kijiweni ukimtukana mjumbe au mwenyekiti tunasema umetukana kijiwe kizima. Hivi Lushinde anapotukana wabunge si kama anatukana jimbo zima?”

Nami sikujivunga. Nilichomekea, “Namkaribisha Lusenge sorry Lushinde aende Kijiweni Mwenge akapige debe au akiweza aende zake gerezani akauze unga. Namshauri Lushinde aje nimuonyesha picha niliyopiga na mzee Matonya ili aone tofauti ya masikio yaliyotobolewa kimila na haya ya kishoga.” wanakijiwe hawana mbavu.

Mgosi Machungi naye hataki kikao kiishe bila kukifunga. Anakula mic, “Mie sikujua kuwa kumbe Ushinde na wenzake wamechanjwa makalioni tena na poofesa Maji Mafupi. Angejua aipotoka kwao N’koogwe akaja Ushoto kue Irente kutafuta wachawi kioo chake kiivunjika akarudi kwa haraka.”

Mpemba “Yaelekea huyu jamaa ashafungwa sana na kufanyia nchezo mbaya kiasi cha kudhani kila aendaye jela afanyiwa nchezo kama alofanyiwa,” kijiwe hakina mbavu.

Mchunguliaji. Msomi mkatatamaa anaamua kurejea ili kutoa usomi na busara zake. Tunamheshimu na kumtegemea sana maana huwa hana mdomo mchafu ingawa leo ameudhika kiasi cha kuvunja mwiko na kutoa lugha ya ukali. Anakatua mic, “Nilipokuwa masomoni ulaya nilizoea kusikia watu wenye midomo mibovu kama hivi wakiitwa Chiwawa yaani vijimbwa vidogo vinavyobweka sana vikimuona mtu lakini akivikaribia vinafyata mkia na kutoka mkuku,”

Anakunywa kahawa yake na kuendelea, “Kwa hiyo sitashangaa kama Chakudema hawatamchukulia hatua chiwawa huyu maana wanajua chiwawa ni chiwawa hata ukimpeleka mahakani bado hakimu atamuachia kwa vile ni chiwawa.”

Mzee Kidevu anatuacha hoi. Anasema, “Ingawa mie sijawahi kwenda Ulaya, anawajua hawa mbwa ambao Kiswahili huitwa kusiri. Hivyo, tuna bahati mbaya kuwa na mbu… samahani simalizii mwenye tabia kama za kusiri. Je, tuseme hiki ni chama cha Makusiri?

Wanakijiwe tunaangaliana kuonyesha jinsi mzee mwenzetu alivyochomekea kitu kingine kwani Kusiri na Chiwawa ingawa wote ni mbwa. Wanakutana kwenye sifa moja yaani uchizi wa kubweka bweka hovyo.

Mpemba ambaye alikuwa akibofyabofya simu yake kiasi cha kuachwa nyuma kimaongezi anastuka na kula mic, “ Yakhe mie naona kama huyu jamaa ashaingiliwa na popobawa. Maana popobawa siku zote aja wakati wa uchaguzi na apenda sana wao wa chama cha Machizi kwani naye chizi.”

Wajumbe hawana mbavu. Wakati tukijiandaa kuendelea na kikao si chizi Lushinde alipita na mshangingi wake. Tuliinuka na kumtoa nje tayari kumfanyizia ili tumpige picha na kuonyesha umma alivyo chakula. Usimwambie mtu, kuwa kweli jamaa si riziki.
Chanzo: Tanzania Daima Aprili 4, 2012.

HOTUBA YA WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII MH. EZEKIEL MAIGE (MB) KATIKA UZINDUZI WA BODI YA WAKURUGENZI YA BODI YA UTALII TANZANIA (TTB)

Mhe.Ezekiel Maige
Ndugu Mwenyekiti wa Bodi, Balozi Charles A. Sanga;
Ndugu Wakurugenzi wa Bodi;
Ndugu Katibu Mkuu, Wizara ya Maliasili na Utalii;
Menejimenti ya Bodi ya Utalii;
Waandishi wa Habari;
Mabibi na Mabwana;
Ni furaha kubwa kwangu kujumuika nanyi leo katika uzinduzi wa Bodi mpya ya Wakurugenzi wa Bodi ya Utalii Tanzania. Napenda kuchukua fursa hii kukupongeza Balozi Charles Sanga kwa kuteuliwa kwako na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Bodi ya Utalii Tanzania ambacho ni chombo muhimu sana katika maendeleo ya sekta ya utalii hapa nchini. Uteuzi huu ni uthibitisho wa imani kubwa aliyonayo Mh. Rais kwako. Aidha nawapongezeni pia Wakurugenzi wote mlioteuliwa kuongoza Bodi ya Utalii Tanzania (TTB).
Hongereni sana!
Ndugu Mwenyekiti,
Kama mnavyofahamu utalii ni moja ya sekta ambazo ni mhimili mkuu wa uchumi ya nchi yetu hivi sasa. Serikali imekusudia kuendeleza sekta hii ili iongeze mchango wake kwenye pato la taifa na maendeleo ya nchi kwa ujumla.
Tangu kuundwa kwa Bodi ya Utalii takriban miaka 18 iliyopita, imeweza kuchangia kuleta mafanikio makubwa katika maendeleo ya sekta ya utalii nchini. Mifano michache ya mafanikio hayo ni pamoja na ongezeko la mapato yanayotokana na utalii kutoka dola za kimarekani milioni 146.84 mwaka 1993, hadi kufikia dola za kimarekani bilioni 1.3 mwaka 2010. Aidha idadi ya watalii imeongezeka kutoka 230,166 mwaka 1993 hadi kufikia watalii 867,994 mwaka 2011. Haya ni baadhi tu ya matunda ya kazi nzuri inayofanywa na Bodi ya Utalii Tanzania, sambamba na taasisi nyingine za umma na binafsi. Napenda kuchukua nafasi hii Kwa niaba ya serikali kuipongeza Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) kwa kazi nzuri inayofanya ya kuitangaza Tanzania kama moja ya nchi zenye vivutio vikubwa na vya pekee barani Afrika na duniani kwa ujumla.
Ndugu Mwenyekiti,
Serikali itaendelea kutoa kipaumbe katika kuhudumia sekta hii, ikiwa ni pamoja na kujenga miundo mbinu, kuongeza bajeti ya utangazaji, kuweka mazingira mazuri kwa wawekezaji, kuboresha huduma kwa watalii kama vile malazi, chakula, usafiri na kadhalika. Nataka nisisitize kuwa ubora wa huduma kwa watalii sambamba na kuimarika kwa utangazaji wa utalii ndani na nje ya nchi ni masuala muhimu katika kuvutia watalii wengi zaidi kuja hapa nchini.
Kwa kuzingatia hilo, Serikali hivi sasa iko katika hatua za awali za kuiunda upya Bodi ya Utalii Tanzania ili kuifanya Mamlaka ya Utalii Tanzania ambapo pamoja na jukumu lake kuu la utangazaji utalii, itawajibika pia kudhibiti huduma na kusimamia shughuli zinazohusiana na utalii, ikiwa ni pamoja na kusajili kampuni za kitalii.
Hatua hii inalenga kukiboresha chombo hiki, kukiimarisha na kukipa nguvu zaidi katika utekelezaji wa majukumu yake.
Ndugu Mwenyekiti,
Ninafahamu kuwa hivi sasa Bodi ya Utalii Tanzania kwa kushirikiana na sekta binafsi ipo katika mchakato wa kutayarisha mkakati mpya wa utangazaji utalii wa taifa. Napenda kuwatia shime katika hili na ninaamini kabisa utekelezaji wa mkakati huu utasaidia sana katika kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea nchi yetu.
Serikali inatambua changamoto zinazoikabili Bodi ya Utalii na hasa ufinyu wa bajeti katika kutekeleza majukumu yake. Kwa sasa Bodi inategemea kwa asilimia mia moja ruzuku kutoka serikali kuu ambayo haitoshelezi mahitaji ya Bodi. Kwa kiasi kikubwa ufinyu huu wa bajeti unatokana na serikali kuelemewa na majukumu mengine katika sekta nyingine kama vile afya, elimu, usafiri, kilimo, na kadhalika. Ni matumaini yangu kuwa changamoto hii itapungua kwa kiasi kikubwa pale utaratibu wa tozo ya kitanda siku utakapoanza.
Ndugu Mwenyekiti na
Ndugu Wakurugenzi,
Mafanikio ya Bodi ya Utalii Tanzania na mengineyo mengi ambayo sikuyataja yametokana na ushirikiano mzuri baina ya Wakurugenzi wa Bodi zilizopita, Menejimenti ya Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) na wafanyakazi wote kwa jumla. Kwa mantiki hiyo, ndugu Mwenyekiti na Bodi yako, ninyi ndio wadau wakuu na chachu ya mafanikio na maendeleo ya Bodi hii. Hivyo naomba nitumie fursa hii kuwakumbusha baadhi ya wajibu na majukumu mliyonayo kwa chombo hiki:
(i) Kuidhinisha mikakati na mipango ya muda mfupi na mrefu ya kutangaza utalii na kuona inatekelezwa ipasavyo;
(ii) Kuidhinisha bajeti za Bodi ya Utalii na kushauri Wizara/Serikali kuhusu mbinu za kuboresha bajeti ya utangazaji utalii;
(iii) Kuishauri serikali juu ya mipango ya kukuza utalii na kuona jinsi Bodi ya Utalii inavyoweza kutoa mchango wake;
(iv) Kuishauri serikali katika masula yanayohusu sera ya utalii, sheria na kanuni zinazohusu ukuzaji na utangazaji utalii;
(v) Kuiongoza Menejimenti katika kukuza maslahi bora ya wafanyakazi waBodi ili kuongeza ari ya kufanya kazi kwa ustadi na ufanisi; na
(vi) Kuwa mlinzi msimamizi (watchdog) katika masuala mbalimbali yanayohusu kukuza utalii na kwa hiyo kukuza pato kutokana na utalii.
Ndugu Mwenyekiti,
Pamoja na majukumu hayo niliyoyataja, ningependa kuwapa majukumu mahsusi katika miaka hii mitatu ya utumishi wenu,msimamie maeneo yafuatayo:
(i) Ningependa kuona kwamba wigo wa utalii unapanuka, zaidi ya utalii wa wanyamapori (wildlife tourism);
(ii) Katika mkakati mpya wa utangazaji utalii, Ni vema suala la 'branding nchi' yetu lisimamiwe na kukamilisha mwaka huu.
(iii) Kuwepo mbinu mpya na za kisasa za utangazaji utalii hii ikiwa ni pamoja na ukamilishaji na utekelezaji wa mkakati wa utangazaji na ukuzaji utalii wa miaka 5 ijayo (TOURISM MASTER PLAN 2012-16) ikihusisha matumizi ya njia za kielektroniki kutangaza (e-Marketing);Lengo liwe ni kufikia watalii million 1 mwishoni mwa 2013 na kuhakikisha utalii unaendelea kukua kwa asilimia 8-10 kwa mwaka na hivyo kufikia walau watalii milioni 1.2 ifikapo 2015.
(iv) Kuboresha mkakati wa uendelezaji na utangazaji utalii wa ndani (Domestic Tourism Marketing Strategy);
(v) Kuiongoza Bodi ya Utalii iwe na vyanzo binafsi vya fedha kupitia vitega uchumi mbalimbali;
(vi) Kuikuza Bodi kama kitaasisi ili kuwa na uwakilishi (mawakala) kwenye Nchi ambazo ni vyanzo muhimu vya watalii. Aidha, ni vema Bodi kusaidia kuanzishwa Bodi ndogondogo za Utalii za Kimikoa na kuwa na maofisa wawakilishi (liason officers) kwenye maeneo hayo ya mikoa. Na,
(vii) Kusimamia vizuri ‘migration’ ya Bodi ya Utalii kutoka ilivyo sasa kama Bodi ya Utangazaji Utalii kwenda kuwa Mamlaka kwa kushirikiana na Idara ya Utalii.
Ndugu Mwenyekiti,
Majukumu haya mnayokabidhiwa leo ni makubwa. Ni matarajio yangu binafsi na serikali kwamba kwa kutumia uzoefu na maarifa mliyonayo na kwa kushirikiana na Menejimenti ya Bodi ya Utalii, mtaweza kukiongoza vema chombo hiki, na mtakuwa kiungo madhubuti baina ya Wizara, Bodi ya utalii, sekta binafsi na sekta ya umma kwa ujumla.
Aidha, naelewa uzoefu, umahiri na weledi mlionao wewe Mwenyekiti na wakurugenzi wengine, ninawafahamu, sijabahatisha kuwateua, hivyo, mkidhamiria hamtaniangusha mimi wala taifa na sina shaka kabisa mtakuwa msaada mkubwa sana kwa Bodi ya Utalii Tanzania. Nyote kwa ujumla mtatumia ujuzi na uzoefu wenu katika kukabiliana na changamoto zinazoikabili Bodi ya Utalii.
Ni matarajio yangu makubwa pia kuwa chini ya uongozi wako ndugu Mwenyekiti, Bodi itaendelea kuimarisha mahusiano mazuri yaliyopo baina ya Bodi ya Utalii na wadau wengine katika sekta ya utalii nchini yataendelea kuimarishwa zaidi kwa manufaa ya sekta hii na Taifa kwa ujumla.
Napenda nikuhakikishie ndugu Mwenyekiti kwamba Wizara yangu itaendelea kutoa ushirikiano kwa Bodi yako ili iweze kutekeleza majukumu haya niliyoyataja hapo juu kikamilifu.
Ndugu Mwenyekiti,
Naomba sasa nitumie nafasi hii kabla sijahitimisha hotuba yangu kuishukuru Menejimenti na wafanyakazi wote wa Bodi ya Utalii Tanzania kwa ushirikiano walioipa Bodi ya Wakurugenzi iliyopita. Ushirikiano wao uliwezesha kufanikisha kwa kiasi kikubwa malengo ambayo walipewa katika kutekeleza majukumu ya kutangaza utalii. Ni matumaini yangu kwamba Menejimenti na wafanyakazi wote wataendelea kutoa ushirikiano huo kwako wewe Mwenyekiti na Wakurugenzi wa Bodi ili majukumu yaliyo mbele yenu yaendelee kutekelezwa ipasavyo.
Ndugu Mwenyekiti na Wakurugenzi wa Bodi, baada ya kusema hayo ninayo furaha kutamka rasmi kuwa, Bodi mpya ya Wakurugenzi wa Bodi ya Utalii Tanzania sasa imezinduliwa rasmi.
Mhe Ezekiel Maige (MB)
WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII
5 Aprili 2012

WAJUMBE WA TUME YA KATIBA

TUME YA MABADILIKO YA KATIBA
(Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, Sura 83,
Toleo la 2012, Vifungu 5, 6 na 7)
______________________________
UONGOZI WA JUU
1.
Mhe. Jaji Joseph Sinde WARIOBA
- Mwenyekiti
2.
Mhe. Jaji Mkuu Mstaafu, Augustino
RAMADHANI
- Makamu Mwenyekiti
WAJUMBE KUTOKA TANZANIA - BARA
1.
Prof. Mwesiga L. BAREGU

2.
Nd. Riziki Shahari MNGWALI

3.
Dr. Edmund Adrian Sengodo MVUNGI

4.
Nd. Richard Shadrack LYIMO

5.
Nd. John J. NKOLO

6.
Alhaj Said EL- MAAMRY

7.
Nd. Jesca Sydney MKUCHU

8.
Prof. Palamagamba J. KABUDI

9.
Nd. Humphrey POLEPOLE

10.
Nd. Yahya MSULWA

11.
Nd. Esther P. MKWIZU

12.
Nd. Maria Malingumu KASHONDA

13.
Mhe. Al-Shaymaa J. KWEGYIR (Mb)

14.
Nd. Mwantumu Jasmine MALALE

15.
Nd. Joseph BUTIKU

WAJUMBE KUTOKA TANZANIA- ZANZIBAR
1.
Dkt. Salim Ahmed SALIM

2.
Nd. Fatma Said ALI

3.
Nd. Omar Sheha MUSSA

4.
Mhe. Raya Suleiman HAMAD

5.
Nd. Awadh Ali SAID

6.
Nd. Ussi Khamis HAJI

7.
Nd. Salma MAOULIDI

8.
Nd. Nassor Khamis MOHAMMED

9.
Nd. Simai Mohamed SAID

10.
Nd. Muhammed Yussuf MSHAMBA

11.
Nd. Kibibi Mwinyi HASSAN

12.
Nd. Suleiman Omar ALI

13.
Nd. Salama Kombo AHMED

14.
Nd. Abubakar Mohammed ALI

15.
Nd. Ally Abdullah Ally SALEH

UONGOZI WA SEKRETARIETI
1.
Nd. Assaa Ahmad RASHID
- Katibu
2.
Nd. Casmir Sumba KYUKI
- Naibu Katibu
Wakuu,
Orodha ya majina ya wajumbe wa Tume ya Katiba hii hapa.
TUME YA MABADILIKO YA KATIBA
(Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, Sura 83,
Toleo la 2012, Vifungu 5, 6 na 7)
______________________________
UONGOZI WA JUU
1.
Mhe. Jaji Joseph Sinde WARIOBA
- Mwenyekiti
2.
Mhe. Jaji Mkuu Mstaafu, Augustino
RAMADHANI
- Makamu Mwenyekiti
WAJUMBE KUTOKA TANZANIA - BARA
1.
Prof. Mwesiga L. BAREGU

2.
Nd. Riziki Shahari MNGWALI

3.
Dr. Edmund Adrian Sengodo MVUNGI

4.
Nd. Richard Shadrack LYIMO

5.
Nd. John J. NKOLO

6.
Alhaj Said EL- MAAMRY

7.
Nd. Jesca Sydney MKUCHU

8.
Prof. Palamagamba J. KABUDI

9.
Nd. Humphrey POLEPOLE

10.
Nd. Yahya MSULWA

11.
Nd. Esther P. MKWIZU

12.
Nd. Maria Malingumu KASHONDA

13.
Mhe. Al-Shaymaa J. KWEGYIR (Mb)

14.
Nd. Mwantumu Jasmine MALALE

15.
Nd. Joseph BUTIKU

WAJUMBE KUTOKA TANZANIA- ZANZIBAR
1.
Dkt. Salim Ahmed SALIM

2.
Nd. Fatma Said ALI

3.
Nd. Omar Sheha MUSSA

4.
Mhe. Raya Suleiman HAMAD

5.
Nd. Awadh Ali SAID

6.
Nd. Ussi Khamis HAJI

7.
Nd. Salma MAOULIDI

8.
Nd. Nassor Khamis MOHAMMED

9.
Nd. Simai Mohamed SAID

10.
Nd. Muhammed Yussuf MSHAMBA

11.
Nd. Kibibi Mwinyi HASSAN

12.
Nd. Suleiman Omar ALI

13.
Nd. Salama Kombo AHMED

14.
Nd. Abubakar Mohammed ALI

15.
Nd. Ally Abdullah Ally SALEH

UONGOZI WA SEKRETARIETI
1.
Nd. Assaa Ahmad RASHID
- Katibu
2.
Nd. Casmir Sumba KYUKI
- Naibu Katibu