Blog yenu ya wananchi yenye habari motomoto za kijamii, Blog yenye kuelimisha, kuburudisha na kufurahisha. Wapenzi na wasomaji wetu tunaomba ushirikiano wenu ili kuendeleza Blog yetu, kwa pamoja tunaweza kuleta mabadiliko ya kweli.

Tuesday, September 24, 2013

Vikosi vya usalama vyaingia Westgate

 23 Septemba, 2013 - Saa 15:32 GMT

Jeshi la Kenya linasema kuwa limedhibiti jengo hilo ingawa hali bado ni mbaya
Milio mikubwa ya risasi na milipuko imesikika huku juhudi za usalama zikiendelea katika jengo la Westgate ambako wanamgmbo wa Al shabaab wameteka jengo hilo pamoja na wakenya wachache ambao wangali kuokolewa.
Kwa mujibu wa waziri wa usalama Joseph Ole Lenku, vikosi vya usalama vimeweza kudhibiti jengo hilo nje na ndani na kwamba ni mateka wachache waliosalia katika jengo hilo.
Serikali inasema watu 62 wameuawa lakini shirika la Red Cross lilisema kuwa idadi hiyo ni 69.
Westgate ni jumba la kifahari lenye maduka na mikahawa karibia themanini .
Milio hiyo ilidumu kwa dakika tatu na kufuatiwa na moshi mkubwa juu ya jengo hilo. Hakuna taarifa kamili kuhusu kilichosababisha moshi huo.
Sehemu ya jengo la Westgate ikitoa moshi
Wapiganaji wa Al shabaab wamewateka nyara raia ambao idadi yao haijulikani. Walikuwemo ndani ya jengo wakiendelea na shughuli zao kuanzia Jumamosi mchana wakati wapiganaji wa Al shabaab walipowavamia na kuanza kufyatua risasi kiholela.
Inaarifiwa kuna maiti kumi katika ghorofa ya kwanza ya jengo hilo.
Aidha wapiganaji hao wanaoaminika kuwa wanachama wa Al Shabaab ni kati ya kumi na kumi na watano na bado wangali ndani ya jengo hilo.
Ripoti zinasema kuwa ufyatulianaji mkubwa wa risasi pamoja na milipuko imesikika katika jengo hilo kwa takriban dakika 15.
Harakati za kuendelea kumaliza operesheni hiyo zinaendelea lakini hali ya mateka walio ndani ya jengo hilo inaendelea kudorora.
Rais Kenyatta amesema kuwa jeshi linajitahidi kuhakikisha kuwa linakabiliana vilivyo na wanamgambo hao.
Wakenya waliofanikiwa kuondoka katika jengo la Westgate kwa usaidizi wa polisi
Helikopta za polisi zinazunguka juu ya jengo hilo pamoja na ndege za kijeshi kushika doria. Vikosi vya usalama vinaendelea na operesheni kujaribu kuwanusuru waathiriwa wakati hali ikiwa ni ya ati ati katika eneo la shambulizi.
Awali jeshi la Kenya lilisema limeweza kudhibiti jengo hilo lote ingawa bado limetaja hali kuwa tete mno hasa katika kujaribu kuwaokoa mateka waliosalia ndani ya jengo hilo.
Ripoti zinasema kuwa watu 69 wamefariki katika shambulizi hilo la Al Shabaab kufikia sasa huku 175 wakijeruhiwa. Baadhi wametibiwa na kuondoka hospitalini. Baadhi ya majeraha waliyopata ni majereha ya risasi na kutokana na guruneti ambalo Al shabaab waliwarushia wale waliokuwa ndani ya mikahawa siku ya Jumamosi.
Kundi hilo limekiri kutekeleza shambulio hilo kutokana na hatua ya Kenya kupeleka majeshi yake nchini Somalia ili kukabiliana na wapiganaji hao.

Chanzo: BBC

No comments:

Post a Comment

Msomaji wetu hakikisha unaheshimu mila na tamaduni za mwafrika,lugha zenye utata au kumkashifu mtu haitapendeza kuonekana kwenye post.Kumbuka vigezo na masharti ya comments kuzingatiwa.Asanteni sana kwa kuwa nasi kwenye blog yenu.