Blog yenu ya wananchi yenye habari motomoto za kijamii, Blog yenye kuelimisha, kuburudisha na kufurahisha. Wapenzi na wasomaji wetu tunaomba ushirikiano wenu ili kuendeleza Blog yetu, kwa pamoja tunaweza kuleta mabadiliko ya kweli.

Tuesday, September 24, 2013

ICC yamruhusu William Ruto kurejea Kenya

 23 Septemba, 2013 - Saa 09:19 GMT

Ruto alifikishwa ICC kwa tuhuma za uhalifu dhidi ya binadamu
Majaji katika mahakama ya kimataifa kuhusu uhalifu wa kivita ICC wameahirisha kesi ya naibu Rais wa kenya William Ruto kwa juma moja ili kumpa mda kurejea nyumbani kushughulikia hali ya kiusalama inayokumba taifa hilo.
Watu wanoaminika kuwa magaidi wa Al Shabaab wameteka jumba la kifahari lenya maduka la Westgate jijini Nairobi na kuwazuilia mateka wakenya kadhaa.

Vikosi vya usalama vyaingia Westgate

 23 Septemba, 2013 - Saa 15:32 GMT

Jeshi la Kenya linasema kuwa limedhibiti jengo hilo ingawa hali bado ni mbaya
Milio mikubwa ya risasi na milipuko imesikika huku juhudi za usalama zikiendelea katika jengo la Westgate ambako wanamgmbo wa Al shabaab wameteka jengo hilo pamoja na wakenya wachache ambao wangali kuokolewa.
Kwa mujibu wa waziri wa usalama Joseph Ole Lenku, vikosi vya usalama vimeweza kudhibiti jengo hilo nje na ndani na kwamba ni mateka wachache waliosalia katika jengo hilo.
Serikali inasema watu 62 wameuawa lakini shirika la Red Cross lilisema kuwa idadi hiyo ni 69.
Westgate ni jumba la kifahari lenye maduka na mikahawa karibia themanini .
Milio hiyo ilidumu kwa dakika tatu na kufuatiwa na moshi mkubwa juu ya jengo hilo. Hakuna taarifa kamili kuhusu kilichosababisha moshi huo.
Sehemu ya jengo la Westgate ikitoa moshi
Wapiganaji wa Al shabaab wamewateka nyara raia ambao idadi yao haijulikani. Walikuwemo ndani ya jengo wakiendelea na shughuli zao kuanzia Jumamosi mchana wakati wapiganaji wa Al shabaab walipowavamia na kuanza kufyatua risasi kiholela.
Inaarifiwa kuna maiti kumi katika ghorofa ya kwanza ya jengo hilo.
Aidha wapiganaji hao wanaoaminika kuwa wanachama wa Al Shabaab ni kati ya kumi na kumi na watano na bado wangali ndani ya jengo hilo.
Ripoti zinasema kuwa ufyatulianaji mkubwa wa risasi pamoja na milipuko imesikika katika jengo hilo kwa takriban dakika 15.
Harakati za kuendelea kumaliza operesheni hiyo zinaendelea lakini hali ya mateka walio ndani ya jengo hilo inaendelea kudorora.
Rais Kenyatta amesema kuwa jeshi linajitahidi kuhakikisha kuwa linakabiliana vilivyo na wanamgambo hao.
Wakenya waliofanikiwa kuondoka katika jengo la Westgate kwa usaidizi wa polisi
Helikopta za polisi zinazunguka juu ya jengo hilo pamoja na ndege za kijeshi kushika doria. Vikosi vya usalama vinaendelea na operesheni kujaribu kuwanusuru waathiriwa wakati hali ikiwa ni ya ati ati katika eneo la shambulizi.
Awali jeshi la Kenya lilisema limeweza kudhibiti jengo hilo lote ingawa bado limetaja hali kuwa tete mno hasa katika kujaribu kuwaokoa mateka waliosalia ndani ya jengo hilo.
Ripoti zinasema kuwa watu 69 wamefariki katika shambulizi hilo la Al Shabaab kufikia sasa huku 175 wakijeruhiwa. Baadhi wametibiwa na kuondoka hospitalini. Baadhi ya majeraha waliyopata ni majereha ya risasi na kutokana na guruneti ambalo Al shabaab waliwarushia wale waliokuwa ndani ya mikahawa siku ya Jumamosi.
Kundi hilo limekiri kutekeleza shambulio hilo kutokana na hatua ya Kenya kupeleka majeshi yake nchini Somalia ili kukabiliana na wapiganaji hao.

Chanzo: BBC

Chenge (Mb) amesema kodi ya kadi za simu (SimCardTax) ni sahihi kwa utafiti wao; aulizwe kupitia 0754782577 atoe maelezo zaidi na vielelezo vya ziada

Posted: 25 Jul 2013 04:35 AM PDT
Leo tarehe 25 Julai 2013 chombo kimoja cha habari kimemnukuu Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti Andrew Chenge (Mb) akisema kwamba uamuzi kuhusu kodi/tozo ya kadi/laini za simu haukuwa wa kubahatisha. Chenge amesema kwamba kamati yake ilifanya utafiti wa kina na kisha kufikia uamuzi wa kuona tozo hiyo ni sahihi.

Ni muhimu akatakiwa kupitia namba yake 0754782577 atoe maelezo zaidi kuhusu usahihi wa tozo hiyo na aeleze ni wapi wananchi na wadau mbalimbali wanaweza kupata vielelezo vya utafiti walioufanya.

Aidha, wenye maswali kuhusu nini hasa kilijiri kwenye kamati ya bajeti mpaka kamati hiyo ikakataa jedwali la marekebisho nililowasilisha tarehe 27 Juni 2013 kabla ya muswada wa sheria ya fedha kupitishwa bungeni tareheb 28 Juni 2013 kwa kuwa yeye ambaye ndiye msemaji wa kamati ameanza kutoa majibu. 

Pia, aeleze iwapo yupo tayari kumshauri Spika aruhusu kamati ya bajeti ikutane kwa dharura wiki ijayo kufanya kazi ya kupitia matumizi ya Serikali kwa lengo la kuanisha maeneo ambayo Serikali inaweza kubana matumizi kwa haraka kufidia pengo la bilioni 178 zinazotafutwa kwenye tozo hiyo ya simu. Hatua hii itawezesha kodi hiyo kuacha kutozwa bila ya kulazimika hata kuongeza vyanzo vingine vya fedha iwapo Serikali inasuasua kupanua wigo wa mapato.

Izingatiwe kuwa katika kuwawakilisha wananchi kuepusha kutozwa kodi ya kumiliki kadi ya simu na nyingine zenye kuongeza gharama za maisha kwa wananchi, kabla ya kupitishwa kwa muswada wa sheria ya fedha nilichukua hatua kuanzia bungeni katika mkutano uliopita wa Bunge.

Niliwasilisha kwa Bunge kupitia ofisi ya Katibu wa Bunge jedwali la marekebisho ya sheria hiyo kwa mujibu wa Kanuni ya 86 (11) ambapo pamoja na mapendekezo mengine nilitaka kifungu katika jedwali la marekebisho la Serikali kilichopendekeza kuanzisha ushuru huo kiondolewe.

Ikumbukwe kwamba kwamba katika mchango wangu kwa kuzungumza bungeni nilisema muswada wa sheria ya fedha wa mwaka 2013 ni “muswada wa majanga” ambao utaleta athari za ongezeko la bei ya bidhaa na huduma muhimu.

Hata hivyo, Kamati ya Bajeti chini ilikataa mapendekezo hayo, hata hivyo kwa kuwa masharti ya kanuni za kudumu za Bunge yanakataza mbunge mwingine kutoa taarifa za majadiliano ya ndani ya kamati sitaeleza kwa undani yaliyojiri katika kikao cha kamati tajwa. 

Hivyo taarifa rasmi na sababu za mapendekezo hayo kukataliwa zinaweza kutolewa na mwenyekiti wa kamati hiyo Mh. Andrew Chenge (Mb) kwa kuulizwa kupitia namba yake ya simu ya mkononi/kiganjani (0754782577).

Uongozi bora na uraia mwema wenye uwajibikaji ni chimbuko na chachu ya ukuaji endelevu wa uchumi wa nchi na ustawi wa maisha ya wananchi.

Kwa ufupi nilielelezwa kwamba tayari chanzo hicho cha mapato na vingine vilishaingizwa katika bajeti ya Serikali kwa ajili ya matumizi ya kawaida na ya miradi ya maendeleo kwa mwaka wa fedha 2013/2014 na kupigiwa kura ya ndio na wabunge wengi kabla ya muswada huo wa sheria ya fedha kujadiliwa. Hivyo nilitakiwa kuwasilisha mapendekezo ya vyanzo mbadala vya kuziba pengo litakalotokana na kufuta ushuru huo na kodi zingine nilizopendekeza zifutwe au zipunguzwe. 

Katika muktadha huo kwa upande wa sekta ya mawasiliano pekee, nilipendekeza vyanzo mbadala vyenye jumla ya zaidi ya bilioni 400 za kitanzania ambazo ni zaidi ya lengo lililowekwa na Serikali bila ya kuongeza mzigo wa gharama kwa wananchi wa kawaida. Nilitoa ushuhuda wa kitakwimu kutoka nchi ya Ghana ambayo makampuni ya simu yanachangia asilimia 10 ya mapato ya nchi hiyo bila kuongeza mzigo mkubwa wa gharama kwa watumiaji wa kawaida wa huduma za simu ya kiganjani/mkononi.

Kati ya mapendekezo niliyotoa ni pamoja na kutaka marekebisho ya Sheria ya Mawasiliano ya njia Kieletroniki na Posta ya mwaka 2009 ili kuipa uwezo wa kutosha Mamlaka ya Udhibiti wa Mawasiliano Tanzania (TCRA) kufanya ukaguzi wa uwekezaji unaofanywa na makampuni ya simu. Hata hivyo, mapendekezo hayo yalikataliwa na kamati ya fedha chini ya uenyekiti wa Andrew Chenge (Mb).

Ifahamike kuwa kwa kurejea masharti ya Kanuni ya 109 (2) niliwasilisha pia katika ofisi kwa Katibu wa Bunge kabla mjadala kuhusu muswada huo kufungwa mapendekezo ya ziada ya vyanzo mbadala vya mapato vya kuziba pengo lililotokana na marekebisho niliyotaka yafanyike kwa lengo la kupunguza mzigo wa gharama za maisha kwa wananchi kutokana na ongezeko la kodi.

Marekebisho hayo yangechangia katika kudhibiti udanganyifu unaofanywa na makampuni mengi ya simu juu ya uwekezaji na faida wanayoipata. Marekebisho hayo yangewezesha pamoja na mambo mengine makampuni mengi kuorodheshwa katika soko la hisa la Dar Es Salaam na pia kudhibiti usajili wa makampuni katika nchi zenye mfumo wa kuwezesha ukwepaji kodi (Tax Heavens).

John Mnyika (Mb)
25 Julai 2013

Waraka kuhusu muswada wa Baraza la Vijana la Taifa wa Mwaka 2013

Vijana wenzangu na wote wenye dhamira ya kuwezesha maendeleo ya vijana nchini, salaam! 

Mtakumbuka kwamba mwezi Januari 2013 nilitoa taarifa kwa umma ya kueleza kuwa niliwasilisha kwa Katibu wa Bunge Muswada Binafsi wa Sheria ya Baraza la Vijana la Taifa na kuomba hatua za ziada toka ofisi ya Bunge kwa kuzingatia Kanuni ya 21 na Kanuni ya 81 ya Kanuni za Kudumu za Bunge. 

Toka wakati huo muswada huo mpaka sasa Mei 2013 haujachapwa katika gazeti la Serikali na nimepokea barua toka kwa ofisi ya Bunge kwamba wamepokea ushauri toka kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuwa muswada huo hauwezi kuchapishwa katika gazeti la Serikali kwa kuwa umekiuka masharti ya ibara ya 99 ya Katiba ya Nchi. 

Sababu ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kutoa ushauri huo ni kuwa muswada unalenga pamoja na mambo mengine kupitia kifungu cha 31 kipengele cha kwanza kuanzisha Mfuko wa Maendeleo ya Vijana kwa madhumuni ya kugharamia shughuli za baraza la vijana la taifa, mipango ya baraza na kutekeleza miradi ya vijana kwa ajili ya maendeleo ya vijana. 

Kwa maoni yangu Mwanasheria Mkuu wa Serikali ametoa ushauri huo bila kuzingatia kwamba kifungu cha 31 kipengele cha pili kinataja vyanzo mbalimbali vya fedha za mfuko ikiwemo kutaja kuwa fedha za mfuko zitatokana na fedha zilizotengwa na Serikali na Bunge kwa ajili ya Baraza kwa mujibu wa Ibara ya 135 kifungu cha pili cha katiba ya Nchi.

Ibara ya 135 (2) ya Katiba ya Nchi inatamka kuwa “fedha ambazo hazitawekwa kwenye Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali ni zile zote ambazo zimetajwa na sheria ya kwamba zitumike kwa shughuli maalum au ziwekwe kwenye mfuko mwingine kwa ajili ya matumizi maalum”. 

Hivyo, ni maoni yangu kuwa ibara hiyo ya Katiba ya Nchi inaweza kutumika kuwezesha kuanzishwa kwa Baraza la Vijana na Mfuko wa Maendeleo ya Vijana bila kufungwa na Ibara ya 99 ya Katiba kifungu cha kwanza ambacho kimeweka masharti kuwa “Bunge halitashughulikia jambo lolote kati ya mambo yanayohusika na ibara hii isipokuwa kama Rais amependekeza kwamba jambo hilo lishughulikiwe na Bunge na pendekezo hilo la Rais liwe limewasilishwa kwenye Bunge na Rais.” 

Kifungu cha pili kinataja mambo yanayohusika na ibara hiyo ya 99 ni pamoja na muswada wa sheria kwa ajili ya “kuagiza kwamba malipo au matumizi ya fedha yafanywe kutokana na Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali au mfuko mwingine wowote au kubadilisha kiwango hicho kwa namna nyingine yoyote isipokuwa kupunguza”. 

Toka Sera ya zamani ya maendeleo ya vijana ya mwaka 1996 itamke kwamba Serikali itawezesha kuanzishwa kwa Baraza la Vijana na suala hilo kurudiwa katika Sera mpya ya mwaka 2007; miaka takribani 17 imepita marais wote wa awamu husika na mawaziri wenye dhamana hawajawasilisha bungeni muswada huo hali ambayo imenifanya niandae muswada binafsi kuwezesha baraza kuundwa. 

Muswada wa Sheria ya Baraza la Vijana la Taifa 2013 niliouwasilisha kwa maoni yangu hauna lengo la kuagiza malipo au matumizi ya fedha yafanywe kutokana na Mfuko mkuu wa Hazina ya Serikali au Mfuko mwingine wowote kwa mujibu wa ibara ya 99 bali unalenga kuanzisha Mfuko wa Maendeleo ya Vijana kwa kuzingatia masharti ya Ibara ya 135. 

Hata hivyo, kwa kuwa muswada huu unahusu mustakabali wa vijana na ni suala la kitaifa kupitia waraka huu naomba kupata maoni yenu kuhusu suala hili, mapendekezo ya marekebisho yanayohitajika kufanyika na hatua zinazopaswa kuchukuliwa. 

Maoni, mapendekezo na hatua hizo zitumwe kupitia mbungeubungo@gmail.com au kwa Afisa wa Ofisi ya Mbunge Ubungo Gaston Garubimbi (0715825025) kabla ya tarehe 24 Mei 2013. 

Nakala ya rasimu ya muswada wa Baraza la Vijana la Taifa wa mwaka 2013 inapatikana katika mtandao wa http://mnyika.blogspot.com kwa ajili ya rejea. 


Aidha, nawaalika kushiriki mikutano ya kupokea maoni kupitia mtandao huo tarehe 20 mpaka 23 Mei 2013 saa 9 alasiri mpaka 10 Jioni ambayo nitashiriki na kutoa maelezo ya zaidi kwa kadiri itakavyohitajika. 

Natarajia kupokea maoni ya vijana na wananchi wengine bila kujali tofauti mbalimbali kwa kuwa madai ya kutaka kuundwe Baraza la Vijana la Taifa yamekuwa yakitolewa na vijana, asasi na taasisi kwa muda mrefu. 

Vyama vya siasa kwa kuzingatia matakwa hayo viliahidi kutekeleza azma hiyo kwa mfano Ilani ya CHADEMA ya mwaka 2010-2015 kipengele 6.4.1 (viii) ilitamka “Kwa kuwa vijana ndio kundi kubwa hapa nchini, na kwa kuwa uhai wa muda mrefu wa taifa letu upo mikononi mwa vijana, Serikali ya CHADEMA itawezesha vijana kuunda Baraza la Vijana (BAVITA) ambalo limekwamishwa na Serikali ya CCM kwa muda mrefu”. 

Kwa upande mwingine, Ilani ya CCM ya mwaka 2010-2015 iliahidi katika kipengele 80 (k) “Kuhamasisha ushiriki wa vijana katika ngazi mbalimbali za maamuzi ikiwa ni pamoja na kukamilisha uanzishaji wa Baraza la Vijana”. 

Mwaka 2011 niliihoji Serikali bungeni ni lini itakamilisha uanzishwaji wa baraza hilo na ikaahidi kwamba kazi hiyo itakamilishwa katika mwaka wa fedha 2011/2012 hata hivyo sasa ni Mei 2013 Serikali haijakamilisha. 

Hivyo vijana, wabunge na wananchi kwa ujumla ni muhimu kuboresha muswada huo na uwasilishwe bungeni kuwezesha baraza la vijana na mfuko wa maendeleo vijana kuanzishwa; maslahi ya umma kwanza. 

Wenu katika uwakilishi wa wananchi,

John Mnyika (Mb) 
19 Mei 2013 
Dodoma
 

Muswada wa Baraza la Vijana 2013-Rasimu ya Kwanza; pakua hapa (download here):
https://docs.google.com/file/d/0B8xvLNf5FlohSHJPX2trR3p6YzQ/edit?usp=sharing