Blog yenu ya wananchi yenye habari motomoto za kijamii, Blog yenye kuelimisha, kuburudisha na kufurahisha. Wapenzi na wasomaji wetu tunaomba ushirikiano wenu ili kuendeleza Blog yetu, kwa pamoja tunaweza kuleta mabadiliko ya kweli.

Sunday, February 19, 2012

Polisi ivunjwe kwa kushindwa uchunguzi sumu ya Mwakyembe-wito

WAKATI Mbunge wa Kyela na Naibu Waziri wa Ujenzi, Dk. Harrison Mwakyembe, analishutumu Jeshi la Polisi kwa kutotimiza wajibu kuhusiana na mambo mbalimbali ikiwamo uchunguzi kuhusu kudhuriwa na sumu, baadhi ya Watanzania wametaka polisi ivunjwe na kundwa upya.
Dk. Harrison Mwakyembe
Baadhi ya Watanzania hao waliotoa maoni yao kufuatia taarifa iliyotolewa na Dk. Mwakyembe, ikibeza na kushangazwa na majibu yaliyotolewa na polisi kupitia Mkurugenzi wa Upelelezi wa Jinai (DCI), Robert Manumba, aliyewaambia waandishi wa habari kwamba “Mwakyembe hakupewa sumu.”
Miongoni mwa wachangiaji hao wametoa maoni yao katika mtandao wa Jamiiforums na wengine katika mitandao mingine ikiwamo tovuti ya gazeti la serikali la Habari Leo lililochapisha habari ikimnukuu DCI Manumba kuzungumzia afya ya Dk. Mwakyembe.
“Ukiona vyombo vya usalama vinacheza na maisha ya raia wake ujue nchi imefika mahali pabaya sana ni suala la muda tu kabla wananchi hawajafikia hatua ya kudai haki zao. Tanzania kupitia Bunge waunde tume yenye lengo la kulifumua jeshi la polisi na kuliunda upya ili liweze kututendea haki Watanzania. Ni aibu kubwa viongozi wakuu wa jeshi la polisi kukubali kutumika kijinga na wanasiasa
DCI Robert Manumba
ambao wana laana ya Watanzania.

“Ni matumani yangu viongozi wa dini, asasi za kiraia watapaza sauti zao ili wale wote waliohusika kwa namna moja au nyingine na uovu huu wanafikishwa mahakamani haraka bila kuchelewa,” anasema Mchangiaji wa muda mrefu katika mtandao wa Jamiiiforums (JF) anayejiita Ngongo.

Mchangiaji mwingine wa JF anayejitambulisha kwa jina la Only83, yeye alianza kwa kumlaumu Dk. Mwakyembe kwa kuendelea kuwa ndani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ambacho kinaendelea kumnyanyasa na kutomsaidia.

“Ninachomlaumu Dk. Mwakyembe ni kuendelea kukaa CCM na kwenye serikali yake wakati wanaendelea kumfanyia vituko…hivi kama wana nia ya dhati ya kumsaidia kwanini wawe na kauli mbili mbili? Hii ni hatari kwa usalama wake. Anapaswa kutambua anapambana na genge kubwa na la hatari. Nashangaa kwa uwezo wake wa elimu na kuchambua mambo anashindwaje kugundua mfumo huu unaomzunguka,” anasema mchangiaji huyo na kuendelea;
“Lakini nadhani polisi na vyombo vya usalama visipuuze hizi habari na kutoa matamko rahisi kama ya DCI Manumba ni kitu kinachoshangaza na kusikitisha.Na hii imekuwa kama mazoea kwa serikali na viongozi wake ni wepesi kutoa majibu rahisi kwa matatizo magumu. Mfano halisi ni huu wa mgomo wa madaktari,Waziri anatoa kauli nyepesi bungeni wakati watu wanakufa. Hii tabia inapaswa kuachwa.”

Mchangiaji katika mtandao wa Habari Leo, yeye alisema;
“Inashangaza kusikia jeshi la polisi kutoa majibu mepesi kiasi hicho wakati malalamiko ya awali ya Dr. Mwakyembe kuhusu njama za kuuwawa na kutaja majina ya watu mpaka gari la polisi na mganga wao wa kienyeji hayajashughulikiwa na hakuna dalili yoyote ya kushughulikiwa na tumeona baadhi ya wanaolalamikiwa wamehamishiwa mikoani ili kuziba ukweli wa kile kinacholalamikiwa. Hatuna jeshi bali tuna kampuni ya mafisadi.”

Mchangiaji mwingine alisema polisi wapo kwa ajili ya kupokea maelekezo tu na siyo kusimamia sheria za nchi akiwafananisha na kompyuta inayosubiri kupewa amri na mtumiaji.

“Tumeshuhudia kesi ngapi zikifutwa pasipo kuwa na sababu, EPA ilipotea mikononi mwa polisi na mahakama, ndio hivyo kwa kupokea maelekezo toka kwa watu fulani ambao ndio wanaoandika katika compyuta,” anasema mchangiaji anayejiita Mizambwa.

Oti Kate yeye anasema, “Mimi nina wasi wasi na uelewa na utayari wa huyu ‘Kayumba’ (Manumba)  katika kujibu maswali.  Katika kujibu swali amesema hivi; Kutokana na uchunguzi wa kipolisi ulioshirikisha Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, hakuna ushahidi juu ya hilo”. ….. baadae  anasema  kazi ya Polisi sio kuchunguza maradhi bali kuchunguza tuhuma, sasa hiyo kushirikisha wizara ya Afya si ndiko wangejua anasumbuliwa na nini? Hapo tayari wizara ya Afya imesha-ridhia kutoa ushirikiano so pamoja na kilichomsibu huyu muheshimiwa…………..dah!”

Katika taarifa yake Jumamosi Februari 18, 2012, Dk. Mwakyembe amesema amekerwa na taarifa ya DCI Manumba kuhusiana na afya yake na kwamba polisi hawajawa na nia ya dhati kuchunguza yanayomsibu.

Taarifa kamili ya Dk. Mwakyembe hii hapa:

“Nimelazimika leo Jumamosi, tarehe 18 Februari, 2012 kutoa taarifa hii kwa vyombo vya habari kufuatia mkutano wa DCI Robert Manumba na waandishi wa habari jana (17/02/12) kuongelea, pamoja na mambo mengine, hali yangu ya afya na kuhitimisha, kienyejienyeji tu kuwa “sikunyweshwa sumu” ila naumwa tu ugonjwa wa ngozi bila kufafanua ugonjwa huo wa ngozi umesababishwa na nini!

“Napenda nisisitize mapema kabisa kuwa msimamo huo wa Jeshi la Polisi umenikera sana katika hali niliyonayo ya ugonjwa, kwanza kwa kuingilia mchakato wa matibabu yangu na uchunguzi wa kina kuhusu kiini chake unaoendelea hospitali ya Apollo nchini India ambako bado sijahitimisha matibabu yangu; pili kwa ufinyu wa uelewa unaojitokeza bayana kwenye tamko la Jeshi la Polisi unaosisitiza kuwa “sikunyweshwa sumu” wakati sumu si lazima unyweshwe ili ikudhuru, inaweza kudhuru hata kwa kugusishwa tu;

“Na tatu kwa Jeshi la Polisi kujiingiza kwenye suala ambalo kwa takriban mwaka mzima halijawahi kuwa na dhamira ya dhati ya kulielewa au kulichunguza mbali na kulifanyia mzaha kupitia magazetini.

“Itakumbukwa kuwa tarehe 9 Februari, 2011 nilimwandikia barua IGP Said Mwema kumtaarifu kuhusu njama za kuondoa maisha yangu na ya viongozi wengine. Kwa kutambua kuwa Jeshi la Polisi la Tanzania daima husisitiza kuletewa ushahidi kwanza ndipo lifanyekazi, nilihakikisha nimeainisha katika barua hiyo kila ushahidi nilioupata au kupewa.

“(Utaratibu huu wa Jeshi la Polisi kusubiri kuletewa ushahidi mezani, kama ambavyo mahakimu wanavyosubiri ushahidi mahakamani, haupo popote pale duniani (ila Tanzania tu) kwani kazi ya msingi ya Polisi si kuletewa, ni kutafuta ushahidi. Polisi wanachohitaji duniani kote ni kupata clue au tetesi tu.

“Hiyo inatosha kufukua ushahidi wote unaohitajika). Pamoja na kujitahidi kuanika kila aina ya ushahidi niliokuwa nao, mambo manne yalijitokeza ambayo yalionyesha wazi kuwa Polisi hawakuwa na dhamira ya dhati ya kupeleleza suala hilo:

(i) Siku chache baada ya kumkabidhi IGP barua hiyo, nilitumiwa timu ya “wapelelezi” ofisini kwangu kuja kuchukua maelezo yangu ya ziada. Timu hiyo ilikuwa inaongozwa na ACP Mkumbo, afisa wa polisi ambaye wiki chache zilizokuwa zimepita alikuwa miongoni mwa askari waliotuhumiwa kupokea rushwa kwa lengo la kumbambikizia madawa ya kulevya mtoto wa Mwenyekiti wa IPP, Reginald Mengi, suala ambalo mpaka leo hii uongozi wa Polisi umeshindwa kulitolea maelezo ya kuridhisha. Kwa msingi huo, nilikuwa nimeletewa mtuhumiwa wa rushwa/ ujambazi kuendesha uchunguzi wa watuhumiwa wengine wa ujambazi! Nikatambua mara moja kuwa zoezi zima lilikuwa la mzaha, tena mzaha mkubwa!

(ii) Wiki chache baada ya barua yangu kuwasilishwa kwa IGP na timu ya ACP Mkumbo “kuanza kazi”, Jeshi la Polisi likachukua hatua ya kuwapongeza na kuwazawadia askari niliowatuhumu kushirikiana na majambazi! Huhitaji kuwa profesa wa falsafa kuelewa kuwa huo ulikuwa ujumbe tosha wa kunipuuza.

(iii) Hivi karibuni tuhuma za askari polisi kujihusisha na vitendo vya ujambazi mkoani Morogoro zilipopamba moto na kuwagusa askari “wale wale” niliowatuhumu kwenye barua yangu, IGP alichukua hatua ya kuwahamishia mikoa mingine!

(iv) ili kunikatisha tamaa kabisa, barua yangu ya “siri” kwa IGP ikavujishwa kwa makusudi kwenye vyombo vya habari na kuchapishwa kama habari ambayo ilikebehi na kukanusha taarifa nzima niliyotoa, sijui kwa faida ya nani! Lakini huu ni mchezo wa kawaida kwa polisi kwani hivi karibuni Mhe. Waziri Samuel Sitta alipohojiwa na ofisa mwandamizi wa Jeshi la Polisi ofisini kwake, wakiwa wawili tu, taarifa ya kikao hicho ikawa magazetini ikikebehi ushahidi aliotoa Sitta! The integrity of the police force leadership is on the line.

Nimeelezea vizuri katika barua yangu kwa IGP kuwa kundi hilo la mauaji lilikuwa limeelekezwa kuniua kwa kutumia sumu, taarifa ambayo kwa karibu mwaka mzima Polisi hawakutaka kuifuatilia kwa sababu wanazozijua wenyewe. Sasa huu msukumo mpya wa Jeshi la Polisi kutaka kujua kama nilipewa sumu au la na kukurupuka kutoa tamko hata kabla ya kunichunguza nilivyo, kunihoji mimi na wasaidizi wangu ofisini na hata kuongea na mabingwa wa Kihindi wanaonifanyia uchunguzi, umetokea wapi?

Aidha napata taabu kuamini kama DCI Manumba na wenzake waliisoma taarifa halisi ya matatibabu yangu au walisoma taarifa “nyingine”, na kama waliisoma taarifa hiyo wenyewe au “walisomewa”! Nasema hivyo kwa kuwa alichokisema DCI Manumba kwa wandishi wa habari hakifanani kabisa na picha iliyo kwenye taarifa halisi ya Apollo ambayo inatamka wazi kuwa kuna kitu kwenye bone marrow kinachochochea hali niliyonayo, kitu ambacho mabingwa wanahangaikia kukidhibiti/ kukiondoa huku vyombo vyetu vya dola vikipelekeshwa na mafisadi kusema bila msingi wa kisayansi na bila aibu: “hakulishwa sumu”, “hakulishwa sumu”!

Nimesoma darasa moja Kitivo cha Sheria Mlimani na DCI Manumba. Baadaye IGP Mwema alikuwa mwanafunzi wangu wa sheria Mlimani. Vigogo hawa wawili wa usalama wa raia nchini hawajanitendea haki, nao wanajua. Wanajua vilevile kuwa sitakaa kimya au kumung’unya maneno come what may pale ambapo haki inakanyagwa.

Tuendelee kuombeana afya na uhai ili kutendeane haki na vilevile tuitendee nchi yetu haki kwa kuvimalizia viporo vinavyokera vya Dowans, EPA, Kagoda n.k. kwa maslahi mapana ya Taifa letu.

Mungu Ibariki Tanzania.

Fikrapevu.com

No comments:

Post a Comment

Msomaji wetu hakikisha unaheshimu mila na tamaduni za mwafrika,lugha zenye utata au kumkashifu mtu haitapendeza kuonekana kwenye post.Kumbuka vigezo na masharti ya comments kuzingatiwa.Asanteni sana kwa kuwa nasi kwenye blog yenu.