Blog yenu ya wananchi yenye habari motomoto za kijamii, Blog yenye kuelimisha, kuburudisha na kufurahisha. Wapenzi na wasomaji wetu tunaomba ushirikiano wenu ili kuendeleza Blog yetu, kwa pamoja tunaweza kuleta mabadiliko ya kweli.

Saturday, February 18, 2012

Nape unasemaje kuhusu falsafa mufilisi ya kujivua gamba?

 
Na Nova Kambota,

  Wapo watanzania wanaoamini kuwa itawachukua muda sana kumsahau mwanasiasa Nape Nauye kutokana na kile kinachoweza kutafsiriwa kuwa jinsi mwanasiasa huyo kijana alivyojigeuza kichekesho kila anapopata wasaa wa kuzungumza na wanahabari naam! Huyo ndiyo Nape Moses Nauye yule katibu wa itikadi na uenezi wa Chama Cha Mapinduzi ambaye amejipachika jukumu la kuitikia kiitikio cha wimbo maarufu wa Jakaya Kikwete wa ``CCM lazima ijivue gamba``.

  Sifahamu mara ngapi huwa Nape anazisoma makala zangu lakini nina uhakika kila anapopata wasaa wa kufanya hivyo huwa hakosi kuzisoma hivyo niweke wazi kuwa nina uhakika makala hii itamfikia iwe kwa kuisoma yeye mwenyewe au kwa kusikia kutoka kwa wapambe wake.

  Ni Nape Moses Nauye huyu ambaye sasa ameamua kupunguza ``uvuvuzela`` baada ya kumaizi kuwa alichodhani ni mapambano kumbe ni fitna za makundi ya ndani ya chama chake. Huyu aliwahi kujitapa kuwa CCM sharti ijivue gamba tena ndani ya siku tisini tu!, wenye akili tulishabaini kuwa hizi ni kelele za mlevi aliyenyimwa pombe, sasa Nape ni shahidi kuwa hivi sasa ni takribani miezi tisa sasa lakini hakuna gamba lililovuliwa au hata hiko chama chake kukiri uzito wa gamba hilo .

   Nape ni aina ya wanasiasa wanaopenda kubebwa kwa mbeleko , hii ndiyo sababu hata alipokuwa anajitokeza na kuzungumza na waandishi wa habari kuhusu dhana ya kujivua gamba kila mwenye akili timamu alijua pasi na shaka kuwa ametumwa na wanaomtumia, alahaula! Lakini Nape kwa kutojua amefuta jina lake kwenye orodha ya wanasiasa wakubwa wa Tanzania wa miaka ijayo, hakuna ubishi naposema kuwa amejifuta mwenyewe naweza nisieleweke , bilashaka hii ni mantiki dhaifu lakini naomba wasomaji wangu muikubali kwasasa licha ya udhaifu wake kwa kuwa pasipo kukubali mantiki hii ya Nape kujimaliza itakuwa vigumu sana kwenu kuuelewa mwelekeo mbovu wa CCM na watendaji wake wa aina ya Nape.

    Labda nitoe mfano wa mwanaharakati na mwanamapinduzi aliyetutoka hivi karibuni hayati Regia Mtema ambaye aliwahi kufanya tendo la ujasiri la kuomba msamaha mara Baada ya matamshi yake makali dhidi ya wale aliowaita ``wafugaji wavamizi`` huko katika wilaya ya kilombero, nachotaka kukisema hapa in ule ujasiri wa Regia kujitokeza hadharani na kuomba msamaha ndiyo maana namuuliza Nape anangoja nini kuomba msamaha kwa kuwaghilibu watanzania? Si Nape aliyejifanya mafisadi watang`oka ndani ya siku tisini? Si Nape aliyewapotezea muda wananchi masikini wa nchi hii kwa kuwadanganya kila uchao? Anataka mpaka Kikwete amtume kuomba msamaha?.

  Ni dhahiri pasipo shaka yoyote kuwa falsafa yaw kujivua gamba imefeli hata mwasisi wake Luteni Kanali Jakaya Mrisho Kikwete anafahamu ukweli huo, tatizo lililopo ambalo linazidi kuimaliza CCM ni kuwa si Kikwete wala huyo Nape aliyetayari kukiri hadharani kushindwa huko, ndiyo maana kwa kutambua hilo nataka kumuuliza Nape kuwa baada ya kushindwa kutimiza alichowaahidi watanzania, sasa anasema nini kuhusu falsafa mufilisi ya kujivua gamba?  Tafakari!, A luta continua!

Nova Kambota ni mchambuzi wa maswala ya kisiasa , Mwanaharakati na Mwandishi wa kujitegemea, anapatikana  kwa anwani ya barua pepe novakambota@gmail.com, au tembelea tovuti yake www.novakambota.com

No comments:

Post a Comment

Msomaji wetu hakikisha unaheshimu mila na tamaduni za mwafrika,lugha zenye utata au kumkashifu mtu haitapendeza kuonekana kwenye post.Kumbuka vigezo na masharti ya comments kuzingatiwa.Asanteni sana kwa kuwa nasi kwenye blog yenu.